#BUFE LA IMANI NA UKRISTO HALISI

Muda mrefu nimekuwa katika fikra na hili limekuwa jambo gumu na kubwa ndani yangu huku imani katika kristo ikiwa ndio chachu kuu katika hili.  Nami nikawa najiuliza kwa muda sasa ya kuwa imani halisi ni ipi ipaswayo kufuatwa, kwa sababu wengi sasa wanakata tamaa zaidi hata kabla ya vile walivyokuwa wanajihusisha na makanisa ya kiroho, na wengine vijana kwa wazee wamethubutu hata kurudi nyuma na kufuata  makanisa ya awali waliyoanza kusali kabla ya kuwa na utashi huru yaani kule mababa zao na mama zao walikokuwa wanasali, hii ni hali halisi kabisa kwa kanisa la Mungu la Tanzania. Nami moyoni hili hunisononesha sana, na hujiuliza hivi je imani ya mwanadamu yaweza  kukuzwa ama kuuawa sababu ya kanisa mtu asalipo? Na’ je kushuka ama kupanda kiroho/kiimani huwa ni kwa sababu ya kanisa, ama mtu mwenyewe ama mchungaji na viongozi wengine wa kanisa?
Na je Imani ni nini hasa?, Biblia inasema Imani ni hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana (Waebrania 11:1). Hivyo imani ni kule kufumbua fumbo, mwanzoni kuna uwezekano mkubwa mtu kuamini kwa namna ambayo inakinzana na maana halisi ya Mungu mwenyewe jinsi alivyotaka.  Ndio maana utaona katika warumi 8:14 biblia inasema wanaoongozwa na roho mtakatifu hao ndio wana wa Mungu, kuna changamoto hapo, maana yake ni kwamba pasipo yeye unaweza toka nuruni na kwenda gizani hali ungali na shauku (Luka 11:35-36) hata pasipo kujua saa ingine (1 Wakorintho 10:12). Na katika waebrania 10:38 ameweka hadharani kabisa “lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani; naye akisitasita roho yangu haina furaha naye”.
Ndio maana somo hili ni bufe la imani ikimaanisha imani ni nyingi duniani na nafsi ya mtu huchagua kwa kuamini; na ni kivipi kuamini; kwa maana mtu ni nafsi huru kama biblia inenavyo na Ukristo halisi ni kwa neema ya wokovu ipatikanayo kwa kumuamini Yesu kristo. Yesu katika biblia anafafanua kuhusu suala la imani, katika Luka 18:7-8 Yesu anasema; Na Mungu je’ hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku? Naye  ni mvumilivu. Nawaambia, atawapatia haki upesi, walakini atakapokuja mwana  wa Adamu, je ataiona imani duniani?. Ona hapo anasema kwa habari yake mwenyewe kama nabii ya kwamba je atakapokuja duniani ataikuta imani. Imani ipi sasa? Anamaanisha ILE IMANI ambayo yeye aliiacha duniani, usemi wake huo unaonyesha shaka aliyonayo juu ya wanadamu na misimamo yao juu ya Imani halisi katika yeye. Na ndio maana Ufunuo 3:11 inaanza kwa kusisitiza ‘naja upesi’ shika sana ulichonacho asije mtu akaitwaa taji yako, hivyo imani hupokelewa na mtu na hupaswa kutunzwa na kuitetea isife ndani ya mtu huyo. Biblia katika Yohana 17:3 anasistiza kuwa; “uzima wa milele ndio huu, wakujue wewe (MUNGU wa pekee wa kweli) na Yesu Kristo uliyemtuma”. Hiko ndio chanzo cha imani yetu kama wakristo yaani kumuamini Mungu na Yesu Kristo aliyetumwa kwetu.
1 wakorintho 13:9 inasema“kwa maana tunafahamu kwa sehemu; na tunafanya unabii kwa sehemu”,  ingawa sasa katika uhalisia mwanadamu kwa hiyo sehemu anayoifahamu hudhani anajua  yote. Cha msingi mtu kujua ni kwamba dini ya kweli ni ile kweli ya Mungu, ambayo mtu huiamini au hupaswa kuiamini.
Mungu wa kweli; hata mashetani wanamfahamu, wanamwamini na hata wakimuona au kusikia jina lake wanatetemeka (Yakobo 2:19), hivyo udhihirisho wa imani yako kule kumwamini Mungu hudhihirishwa na matendo yako, sasa kutotenda sawa sawa ni dhahiri kwamba imani ndani ya mtu huwa imehadaiwa. Kwa maana imani chanzo chake ni kusikia; na kusikia huja kwa neno la kristo (warumi 10:17), kwa hivyo imani chanzo chake lazima mtu asikia neno la Mungu, vinginevyo ni upotofu.  
Imani nyingi zinazoelezwa kuenea ni kutokana na wapinga kristo wengi ambao wamekwisha kuwapo duniani (1 Yohana 2:18). Tatizo sasa kuhusu ukristo halisi na hili suala la bufe la imani sio juu ya wachungaji ama kanisa bali mtu mwenyewe, maadamu biblia imeeleza uwepo wao. Suala ni mtu mwenyewe; anatakiwa asikie neno la kristo ndipo aamini na sio maneno mengine na kumuamini Mungu pekee yake na Yesu kristo aliyetumwa kwetu na sio kingine. Na ijulikane kabisa wokovu ni kwa neema na ni Baba wa mbinguni ndiye humuokoa mtu na wala si mwanadamu. Hatuendi tu kwa Mungu bali yeye hutuvuta kwake kwa neema yake, ila sharti tuamini kwamba Mungu yuko (waebrania 11:6).
Na tamaa zako sio kipimo kwamba unampenda Mungu, (1 Yohana 2:16-17) hata kama utakuwa unaenda kanisani, hivyo shauku yako huangaliwa kama kweli unamwamini Mungu wa kweli, nia ya mtu kwa Mungu ndio hupelekea mshikamano na Mungu, kama sivyo basi ni tamaa na tamaa ya vya dunia huvita vya dunia (Warumi 1:24) ikiwa pamoja na imani za wapinga kristo. Uhakika ni huu ya kwamba ukimwamini Mungu wa kweli huwezi potea njia kwa maana nia yako na mawazo yako yatakuwa wazi mbele zake na matendo yako kuthibitika naye hatakuacha upotee milele. Na biblia katika 1 Yohana 2:17 inathihirisha ya kuwa mwanadamu atadumu hadi milele kwa kuyafanya mapenzi ya Mungu.
Biblia katika Efeso 1:3 -7 inatuhakikishia kuwa wokovu uliojua ndani yako ni halisi kabisa, na ndiye kristo kwa neema yake alikujalia kuwa nao na ndiye aliyetuchagua kabla ya kuwekwa misingi ya ulimwengu. Kwa hivyo wokovu ni wa mtu binafsi ila sasa unaokolewa na Bwana ili uokoe wengine kuanzia na familia yako yaani watu wa nyumbani mwako, umeokolewa ili kutangua misingi ya vizazi vya kale iliyo kinyume na kusudi la Mungu duniani na kuvunja madhabahu za miungu ya ukoo na kujenga misingi mipya na madhabahu mpya inayomtii na kumuamini Yesu Kristo ya kuwa ni Mungu pekee asitahiliye kuabudiwa na kila kiumbe. Kama Gedioni katika waamuzi 6 pale alipookolea tu na Bwana akatangua madhabahu ya baba yake na mababu yaani zile madhabahu ya miungu kwa maelekezo ya malaika wa Bwana akatoa dhabihu kutangua dhabihu za damu za watu na wanyama zilizomwaga katika madhabahu zile, na kisha akafanya madhabahu mpya kwa dhabihu safi ili Yesu kristo atukuzwe kwenye ule ukoo na jamii kwa ujumla na ikawa hivyo.
Yesu kristo alikuja na agano jipya ndio! Lakini kuwapo jipya hakukufutilia mbali lile la kale alilifuatilia kwa kina na kutangua panapostahili na kukazia palipopaswa kuondoa mapungufu yote ili kuwepo ukamilisho katika lile lililo jipya. Niseme nini sasa, wokovu ni uhuru wa nafsi ya mtu katika dunia ile ile iliyo na uovu ambao bado unakuwa unafuatilia nafsi ile ile iliyowekwa huru na Bwana, Ndio! Nimeokoka ila ukoo wangu bado, hapo jua kuna kazi ya kufanya ili uhuru wako uwe kweli na hakika, wokovu wako hauna taji kama hauthihirishwa au kupimwa kwa kazi uliopaswa kuifanya.
Imani ni nyingi duniani, na kuna ukristo halisi na imani halisi kabisa ambayo Bwana Yesu Kristo aliikusudia, na ndio maana hata mwanzo wa huduma alionyesha mzigo aliokuwa nao juu ya imani zilizokuwa ni kama zinawafunga zaidi kondoo badala ya kuwafungua na kuwafanya huru, na ndio maana hata tamko la Isaya 61:1 alilisema kanisani na sio njiani wala sokoni bali hekaluni mwa Mungu kondoo wanakokusanyika na kusikia Neno la Mungu. Na ye Yesu wa Nazareti alisema Roho ya Bwana MUNGU i juu yangu; kwa sababu Bwana amenitia mafuta niwahubiri wanyenyekevu habari njema; amenituma ili kuwaganga waliovunjika moyo, kuwatangazia mateka uhuru wao, na hao waliofungwa habari za kufunguliwa kwao. Hili tamko ni kubwa sana ina maana waliofungwa walikuwepo kanisani, waliovunjika mioyo walikuwepo kanisani na mateka walikuwepo pia. Na sasa wapo kondoo waliokuja na vifungo hivyo lakini pia wapo ambao vifungo vilizidishwa hapohapo kanisani walikojua ni msaada kwao, kutokana na jinsi walivyojengewa imani na viongozi wachungaji wa kanisa ama kutokana na Neno la Mungu jinsi vile walivyokuwa wanafumbuliwa, kuaminishwa ama kutafsiriwa..... Si la kushangaza sana hata Yesu wa Nazareti pale alivyowaita mafarisayo, masadukayo, waandishi, waalimu wa sheria kuwa ni wanafiki! Kwa kuwa wanafanana na makaburi yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yanaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu, na uchafu wote (Mathayo 23:27).
Ndugu mpendwa katika Bwana; Ukristo halisi na imani isiyo na ukengeufu ni kuongozwa na ROHO MTAKATIFU huko ndiko kutakufanya wewe uwe MWANA WA MUNGU (warumi 8:14) na uishi kama MFALME katika hii dunia, Barikiwa na Bwana Yesu Kristo, Amina.


No comments:

Post a Comment