#NENO LA MUNGU NI NGUVU JITABIRIE YALIYO MEMA

       Maneno yanaumba siku zote jitabirie yaliyo mema, wala kujitabiria sio tu kwa manabii na waonaji, wana wa Mungu yawapasa kujitabiria na kujinenea yaliyo mema juu ya maisha yao, vitu vizuri, maisha mazuri lakini ikiwemo imani ndani ya ukiri wao kupitia maombi ya nguvu katika jina la Yesu kristo. Tunaona jinsi Neno la Mungu lilivyo nguvu, katika 2 wafalme 7:1 Elisha alitamka kwa imani ya kwamba kesho muda na saa kama hii kipimo kizuri cha unga kitauzwa kwa shekeli na vipimo viwili vya shayiri kwa shekeli langoni pa Samaria, nasema Neno la Mungu ni nguvu kwa sababu kwa namna yoyote ile litatimia, likishatamkwa haijalishi mazingira, litathibitika vipi? Itakuwaje kuwaje? Mungu mwenyewe anajua yupi atakuwa punda kulithibitisha lakini ni lazima lithibitike kwa kuwa ni Neno la imani na kwa imani limenenwa na ni Neno la Bwana. 

Ni wosia wa Mungu katika jina la Yesu ya kwamba tuishi maisha katika mtindo huu wa kukiri yaliyomema juu ya maisha yetu na ikawa hivyo kwa sababu alikufa msalabani ili wosia (Neno la Mungu) uweze kuwa halisi uthibitike na kutenda kazi katika maisha yetu. Unajua Adam hakutamkwa kama Nabii katika Biblia bali mtu ambaye Mungu alimuumba kwa mfano na sura yake lakini aliweza jitabiria juu ya maisha yake vyovyote alivyotaka na ikawa na pia Mtu wa Mungu Enoch hakuitwa Nabii lakini alifanya hivyo, hiyo yote ni kwa sababu huu ndio wosia wa Mungu kwa mwanadamu aliye na sura na mfano wake Mungu. Ndio maana katika wafillipi 4:13 inasema “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu”, mambo yote! Je’ yapi magumu ya kumshinda Bwana?. Biblia inasema katika Kitabu cha mwanzo 1:26; kuwa Mungu alimfanya mtu kwa mfano wake na sura yake ili atawala vyote viijazavyo dunia. Mwanzo 2:19 inasema Mungu akafanya wanyama na ndege akamletea adam aone atawaitaje (hapa alimjaribu kama ataweza) biblia inasema jina lolote alilompa mnyama na ndege likawa ndio jina lake (yaani chochote alichosema kikawa ndiyo hivyo), hivyo aliweza jaribio hilo na Mungu akaona ni vema, yuko katika mfano na sura yake kwa kuwa anaweza kufanya kama yeye, akamwamuru kutawala vyote duniani ikijumlisha shetani na uzao wake yaani kama mfalme wa dunia kwa kuwa nguvu na mamlaka ya Mungu yalikuwa ndani yake.Jua kwamba wanadamu hatupo kumjaribu Mungu kama kweli ni Mungu bali yeye hutuangalia sisi kama kweli tunaishi kama miungu duniani(Zaburi 82:6).Yesu alitukumbusha nafasi yetu katika dunia hii; kwa kusema “mnavyosali semeni Baba yetu ulie mbinguni, jina lako litukuzwe, ufalme wako uje…” neno ufalme wako uje linaashiria kuwa ufalme wa Mungu wa sisi kutawala na kumiliki dunia, ambapo kwa kutokujua kwetu shetani anatutawala na hali neno mfalme ni mtawala na kuhani ni mimiliki baada ya Yesu kujifunua kwetu. Hivyo kwa sala hiyo ya Baba yetu alitaka tujue kuwa ufalme unatuhusu na unatakiwa ukae ndani yetu ili tuwe wafalme, je umetambua ndugu?. Mwambie shetani ya kwamba unastahili na unasifa na uweza wa kushika nafasi hiyo ya ufalme katika kristo Yesu na ya kwamba wewe ni mkuu na sio mtumwa wa shetani bali yeye ndiye mtumwa wako mpaka siku ya kiama.

Mwanzo 2:21-23 inasema jinsi Mungu alivyomfanyia mwanamke Adam kutoka katika ubavu wake baada ya kumpa usingizi mzito Adam na kisha akamletea Adam. Adam alivyoamka,” akaanza kusema huyu ni mbavu na mbavu zangu na nyama ya nyama yangu naye ataitwa mwanamke kwa sababu alitolewa kwa mwanamume, kumbuka wakati Mungu anatenda yote hayo Adam alikuwa katika usingizi mzito lakini cha ajabu alipoamka alijitabiri yaliyo ya kweli kuhusu mwanamke ikawa ndiyo hivyo ilivyokuwa. Mfalme Sulemani anasema katika mithali 18:21 “Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi; Na wao waupendao watakula matunda yake”. Siku zote nitachagua na kupenda uzima kwa kunena uzima kwa ulimi wangu, kwani Ulimi unauwezo wakutamka uzima katika kila kitu na vikawa kwangu, hivyo utakuwa ndio wimbo wangu katika midomo yangu na nitatamka uzima, nitajinenea mema na kujitabiria vitu vizuri vitokee maishani mwangu kwa maana ndiyo matunda niyahitajiyo. Najua nafasi yangu mimi ni kuhani, mimi ni mfalme nguvu na mamlaka ya dunia nzima vipi chini yangu katika jina la Yesu kristo hatua kwa hatua nitamiliki na kutawala. Na sitasema na kuimba ufalme uje hali naamini kupitia kristo yesu ufalme upo ndani yangu moyoni mwangu na nafsi mwangu. Biblia inasema tafuteni kwanza ufalme wa Mungu na wengineyo utapewa kwa ziada, mwana wa Mungu sema nahitaji hivyo vyote vilivyo vya ziada mbele za Mungu ile hazina iliyositirika na utajiri ulioficha sirini nipewe mimi sasa na niumiliki (Isaya 45:3) kama vile Mungu wangu anayenijua kwa jina langu alivyoniahidia, ambapo shetani kwa kule kutokujua kwangu ameushikilia. Mimi ni mwana wa Mungu mrithi pamoja na Yesu Kristo, jitabirie na kujitamkia sasa! Katika maisha yako vitu vizuri na sio vitu vya kufa vile vya kukatisha tamaa, jinenee vile vyote ambavyo unataka viwepo katika maisha yako hapa duniani kwa sababu Mungu wetu sio Mungu wa vitu vya kufa au vilivyokufa bali Mungu wa viishivyo vyenye uhai na vinavyotokea, Amina! Barikiwa na Bwana katika jina la Yesu Kristo. Amina

No comments:

Post a Comment